Sunday, March 15, 2015

CWT: JIBU RAHISI KWA MASWALI MAGUMU!





CWT ni trade union iliyo mstari wa mbele kuhakikisha walimu hapa nchini wanapata stahili zao kwa wakati.Pamoja na ukweli kuwa CWT imejitahidi sana katika kutekeleza wajibu huo bado CWT ina mapungufu kadhaa ya kimuundo na kiutendaji. Makala hii inajadili maswala yahusuyo uanachama, makato ya ada ya uanachama na muundo wa benki ya walimu kuelekea katika uchaguzi mkuu wa CWT.

Nimekuwa nikiandika mara nyingi kuhusu uanachama wa mwalimu katika CWT. Katiba ya CWT inasema wazi kuwa kuna aina tatu za wanachama wa chama hicho, mosi ni wanachama wa heshima ambao hupewa uanachama kutokana na mchango wao kwa CWT,Aina ya pili ni uanachama wa hiari na tatu ni wanachama wa halisi ambao wanatoa ada ya uanachama kila mwezi.Upungufu uliopo katika kipengele cha wanachama ni katiba kutotoa maelezo ya kutosha kuonyesha namna ya upatikanaji wa hao wanachama halisi.

Makato ya ada ya uanachama ni upungufu mwingine wa CWT. Tangu nimeifahamu CWT haijawahi kuwa na kiwango sawa cha makato ya ada ya uanachama kwa wanachama wake.CWT imekuwa ikikata 2% ya mshahara wa kila mwalimu kila mwezi kama ada ya uanachama. Kwa maswala hayo mawili ya uanachama na makato ya ada kwa asilimia 2% ya mshahara wa mwalimu kila mwezi ni tatizo linalohitaji ufumbuzi wa haraka. Uvunaji wa pesa za walimu isivyo halali kila mwezi na kutufanya tujiulize hivi CWT ni kwa maslahi ya nani? serikali, AU Viongozi wake?

Nasema CWT inavuna pesa za walimu isivyohalali kila mwezi kutokana na ukweli kuwa kwa sheria zilizopo cwt haina mamlaka ya kuchukua ada ya uanachama kwa % ya mshahara wa mtumishi.Nasema hayo kwa kuwa sheria zote tangu ile ya mwaka 1961,"The organisation of Tanzania Trade Union Act,1961, the trade Union(Revocation of special powers) Act,1962,The Trade Union ordiance Act,1962,"The Trade Unions and Trade Disputes (Miscellaneous Provision)Act, 1964 hadi hii ya sasa iliyofanyiwa marekebisho 2006. Hakuna mamlaka ya aina hiyo isipokuwa kwa sheria ya "Employment and Labour Relations Act,2004(4) inayotoa mwongozo wa nini kifanyike kuhusu makato [Si kwa %] ya mshahara kwenda trade union husika. Kwa mantiki hiyo,CWT imekuwa ikuvuna mabilioni ya pesa isivyo halali kila mwaka kutoka kwa walimu pasipo ridhaa yao.


Aidha,siku za hivi karibuni, kila mahali pa kazi kwa walimu gumzo kubwa ni uchaguzi wa CWT. Walimu wanapigana vikumbo kuhakikisha wanapata nafasi ya uwakilishi au uongozi ndani ya CWT.Huo ni upande mmoja wa shilingi. Upande wa pili wengine wanatafakari nini cha kufanya kutokana na CWT  kuweka masharti yanayowanyima fulsa ya kushiriki katika chaguzi hizo.Moja ya masharti hayo ni mwanachama kuwa ametoa ada ya uanachama kwa kipindi cha miezi kumi na mbili mfulululizo.

Swala la kigezo cha ada napenda nilijadili kwa kirefu kidogo. Hapo juu nimeeleza kuwa kuna walimu ambao kimsingi hawajawaridhia makato ya mshahara wao kwenda CWT lakini wamekuwa wakikatwa. Kuanzia septemba mwaka jana baadhi ya walimu hao wameondolewa makato hayo na baadhi wakiendelea kukatwa makato ya ada ya CWT.Pamoja na Viongozi kutambua CWT imekuwa ikipata mgao toka hazina kama makato ya ada ya uanachama kwa walimu hao ambao kwa sasa hawapo katika makato, waliamua kuweka “kizingiti” kwao ili wasipate fulsa ya kuchagua au kuchaguliwa hata kama walikuwa wakikatwa ada kwa muda mrefu kiasi gani. Hii si sawa hata kidogo!Jambo hili linaleta maswali zaidi ya majibu yanayotolewa kiasi cha kufanya wengine tupoteze imani kwa chama. Viongozi wa CWT wanakiri kuwa kuna walimu wameondolewa makato ya ada ya uanachama na njia pekee ya uchangiaji inayotumiwa ni mwajiri kukata mshahara wa mwalimu na kupeleka katika CWT.Ikiwa makato hayo yamesimamishwa. Je ni nani anayewajibika na kusimamishwa huko ikiwa mwalimu hajawahi kuomba kusimamishiwa makato?.Je, ni halali mwalimu kunyimwa haki ya kushiriki shughuli za chama wakati ameshachangia zaidi ya miaka kumi?Ikiwa alikuwa amekatwa kimakosa,[kama hajawahi kuridhia makato hayo] Je,kwanini chama kisirejeshe  makato hayo kwa mwalimu?.Je,ni hatua gani CWT imechukua baada ya kuona mapato yatokanayo na ada za uanachama yamepungua? Je, CWT haioni kuwa si sahihi kumzuia mwalimu aliyechangia kushiriki katika shughuli za chama?

Uanzishwaji wa benki ya walimu ni wazo zuri ninaloliunga mkono.Viongozi wa CWT  wanapita maeneo ya kazi kuhamasisha walimu kununua hisa ili umiliki wa benki hiyo kwa sehemu kubwa uwe chini ya walimu. Aidha, taarifa zinaeleza kuwa kila mwanachama hai wa CWT atanunuliwa hisa kupitia michango yake ya kila mwezi aliyoyochangia. Hofu yangu bado ipo kwa walimu ambao wameondolewa katika makato hayo.Je, hawa hawana haki ya kushiriki pia katika shughuli za benki ya walimu? Vipi kuhusu hatma na thamani ya michango waliyokwisha changia CWT?. Tunahitaji majibu yenye mashiko kutoka CWT.

Naandika  makala hii kwa CWT na walimu kwa ujumla kwa kuwa naamini kwamba kitendo cha kuwanyima fulsa walimu kushiriki kikamilifu katika shughuli za CWT ni jibu rahisi kwa maswali magumu. Naamini walimu ni waelewa na wenye hekima.Nao watatumia busara zao kulitathimini jambo hili na kulitafutia ufumbuzi. Aidha ,nawaandikia watanzania kwa kuwa naamini kuwa wao ni watu makini na wenye busara ambao hawapo tayari kuona uonevu ukifanywa katika jamii yao.

Sunday, February 20, 2011

Mpango wa MWAKEM: “Usiwe Jibu rahisi kwa tatizo kubwa !”

Dec, 16, 2010 taasisi ya uwezo Tanzania ilitangaza matokeo ya utafiti wake kuhusu uwezo wa watoto kusoma na kuandika nchini Tanzania. Katika utafiti huo, imebainika kuwa idadi kubwa ya watoto nchini hawawezi kufaulu majaribio kwa kiwango kilichotarajiwa. Matokeo ambayo kimsingi yanatoa wito wa kuboresha ufundishaji na ujifunzaji katika kila somo.


Kwa muda mrefu sasa, jamii imekuwa ikiwatupia mzigo mkubwa wa lawama walimu pindi ufaulu wa wanafunzi unapo kuwa duni. Kimantiki lawama hizo zinaweza kuwa na mashiko. Hii inatokana na ukweli kuwa ubora wa elimu itolewayo unategemea sana uwepo wa walimu wenye sifa,vifaa vya kufundishia na kujifunzia, mitaala thabiti na thahili,ushirikiano wa walimu, wanafunzi, wazazi,wadau wa elimu na tathmini sahii ya mtaala inayokubalika.

Kwa kutambua kuwa ubora wa walimu ni kigezo muhimu cha msingi katika kuinua ubora wa elimu, Wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi ili kukidhi mahitaji katika utekelezaji wa mpango wa maendeleo ya sekta ya elimu (ESPP)ambao ilihusisha mipango kabambe ya MMEM na MMES iliandaa mkakati wa menejimenti na maendeleo ya walimu MMEMWA ili kuimarisha ubora wa elimu ya ualimu. Hii ilitokana na ukweli kuwa mafanikio ya mipango yote miwili MMEM na MMES litegemea sana upatikanaji wa walimu.

Aidha, kwa kutambua kuwa mafunzo ya walimu kazini ni nyenzo kuu ya kufanikisha ubora wa ufundishwaji na ujifunzaji darasani.Serikali imeamua kuimarisha programu za mafunzo kazini kwa walimu .Kuanzia Julai ,2010, wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi ilianza kutekeleza mkakati wa mafunzo kazini kwa walimu wa shule za msingi ngazi ya shule-MWAKEM kwa lengo la kuinua ubora wa walimu wa shule za msingi katika kufundisha elimu ya awali na msingi kwa ufanisi.

Ni dhahiri kuwa ikiwa mpango huu utaratibiwa na kusimamiwa vema walimu watapata kujifunza mambo mapya kama vile mabadiliko ya mitaala, dhana na nadharia za ufundishaji na ujifunzaji na hivyo kuweza kukabiliana na changamoto za mabadiliko katika elimu kila wakati.

Kwa mujibu wa mwongozo wa usimamizi na utekelezajimwam MWAKEM uliotolewa novemba 2010,usimamizi na uendeshaji wa mafunzo kazini kwa walimu wa shule za msingi ngazi ya shule umeelekezwa vizuri sana.Aidha,watendaji wakuu katika utekelezaji huo na majukumu yao katika kila ngazi wameainishwa vema.Na kwa lengo la kuwa na mafunzo yenye ufanisi na endelevu kwa walimu mafunzo hayo yameandaliwa kutolewa kwa kushishikiana na halmashauri za wilaya.

Nashawishika kuuona mpango wa MWAKEM kuwa ni jibu rahisi kwa tatizo kubwa kwa sababu kuu mbili; mosi ni uzoefu unaotokana na utekelezaji wa mipango iliyotangulia na pili ni pengo kubwa lililopo kati ya ukweli wa hali ya elimu yetu na jitihada za mantiki tunayotumia ili kuuona ukweli huo katika kutathimini na kuinua ubora wa elimu nchini.

Utekelezaji wa mipango mingi ya maendeleo ya elimu iliyotangulia umekuwa na changamoto nyingi sana.Mfano mzuri katika kuelezea hili ni mpango wa mafunzo kazini kwa walimu wa daraja la tatu B/C-A mpango uliokuwa maarufu sana kwa jina la “moduli”. Utekelezaji wa mpango huo ulikumbana na changamoto nyingi sana.Kubwa miongoni mwa changamoto hizo ilikuwa ni utayari wa walimu tarajiwa kujiendeleza kuwa mdogo na halmashauri nyingi kutotenga fungu kwa ajili ya mafunzo kabilishi na yale ya ana kwa ana kati ya wakufunzi na walimu ili kutathimini maendeleo ya walimu katika kujifunzaji. Kwa mujibu wa mwongozo wa utekelezaji wa MWAKEM kila halmashauri imeelekezwa kutenga pesa kiasi cha tsh elfu arobaini [40,000/=] kwa kila mwalimu kwa ajli ya mafunzo hayo kila mwaka katika bajeti yake.Uzoefu unaonyesha kuwa halmashauri nyingi kipaumbele chao huwa sio maendeleo ya taaluma ya walimu na ndio maana mafungu hayo huwa hayapo na ikitokea yakatengwa huwa yanatumika kwa shughuli nyingine tofauti na malengo tarajiwa.Tatizo linaloonekana kuwa sugu.

Nimelazimika kutolea mfano mpango wa C/B-A na MWAKEM kwa kuwa wahusika wakuu katika utekelezaji wake ni wale wale na mfumo wa uendeshaji wake hauna tofauti na ule wa C/B-A ambao mafunzo yake yalitolewa kwa njia ya masafa kupitia moduli.

Sababu nyingine inayonifanya kuuona mpango huu ni jibu rahisi kwa taizo kubwa kama nilivyodokeza hapo awali ni pengo kubwa lililopo kati ya ukweli halisi wa hali ya elimu yetu na jitihada za mantiki tunayotumia ili kuuona ukweli huo katika kutathimini na kuinua ubora wa elimu nchini.Kwa mfano,ni ukweli usiopingika kuwa mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji darasani unategemea sana umahiri wa mwalimu.Ni udhaifu mkubwa ikiwa tutakuwa tunazungumzia mpango wa kumpata mwalimu “mahiri” pasipo kueleza njia na vigezo tutavyotumia katika kumpata na jinsi ya kumfanya auishi umahiri wake.

Napenda kuwakumbusha wadau na wanaharakati wa elimu kuwa ubora wa elimu ni zaidi ya kuwa na mwalimu “mahiri” kwani hutegemea sana uwepo wa mitaala thabiti na dhahiri,uwepo wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia, walimu wenye sifa,miundombinu inayovutia ufundishaji na ujifunzaji na ushirikiano wa wazazi,walimu,wanafunzi na wadau wote wa elimu.

Aidha napenda kuwakumbusha pia kuwa pamoja na ukweli kuwa elimu yetu inachangamoto nyingi,bado mafunzo kazini kwa walimu ni ya lazima na yanayopaswa kuwa endelevu.Ikiwa mifumo ya uendeshaji na usimamizi itaimarishwa ni dhahiri kuwa kiwango cha ufundishaji wa walimu wetu kitaimarika na hivyo lengo la taifa la upatikanaji wa elimu bora kwa wote litafanikiwa.





MTOTO WA MKULIMA: Msamiati uliotekwa nyara!!!!!!

Harakati za ukombozi wa mwanadamu katika Nyanja zote za kiuchumi,kisiasa,kiutamaduni na kifikra zina historia ndefu.Kutokana hali hiyo ndiyo maana wanazuoni tunashawishika kuamini kuwa historia kwetu ni sasa ikivuviwa na zamani.Ni matendo ya sasa yakitiwa nguvu na yale ya waliotutangulia?!!

Nimeanza makala hii kwa maelezo hayo katika kuutafakari msamiati wa “Mtoto wa Mkulima” ili niweze kuonyesha pengo kubwa lililopo kati ya ukweli wa maisha yetu na jitihada za mantiki tunayotumia ili kuuona ukweli huo.

Msamiati wa “Mtoto wa Mkulima” umeshika kasi ya ajabu sana katika siku za hivi karibuni.Ulipoanza kutumika msamiati huu,watumiaji wake walikuwa wakimaanisha kweli wao ni watoto wa wakulima,watu safi,wenye kuenenda katika mapito safi na waliotayari kupigania maslahi ya wengi.Kutokana na hali hiyo,ndipo wafuasi lukuki wakajitokeza mstari wa mbele katika kuunadi msamiati huo.

Jumuia ya wanachuo wa chuo kikuu cha Dar es salaam ni moja ya maeneo ambayo msamiati wa mtoto wa mkulima umeshika kasi ya ajabu!!!!Wanazuoni kadha wa kadha wakijipambanua kama wanaharakati wamekuwa wakijinadi kama watoto wa wakulima ilihali kihalisia sio kweli-hawako hivyo hata kidogo!! Wamekuwa wakijitokeza mbele ya hadhira mikono nyuma wakiendeleza kile wanazuoni wanachokiita “Vuguvugu la Umajumuni” katika kupinga mifumo dhalimu inayotufanya kuafiki kile tusicho amini.Jambo la kusikitisha ni pale wanapopewa mamlaka/madaraka ya kuwaongoza wenzao ghafla hunaswa katika mikoba ya ya uchawi wa “Giningi” na kusahau kabisa misingi ya harakati zao na kisomo chao kilichowapa nafasi ya kuwa pale walipo. Wanaishia kufanya kinyume na kabisa matarajio ya watu na kuwaacha “ watoto wa wakulima” halisi wakiishi na tamaa zao katika hali ya kukata tamaa!!!?

Binafsi sishangai hali hii kutokea.Sishangai kwa kuwa ni hali niliyoitegemea.Ni hali iliyotegemewa kwa kuwa tangu enzi za uhuru wan chi hii waasisi wake walisema wazi kabisa kuwa hii ni nchi ya wakulima na wafanyakazi.Baada ya wakulima kujipambambanua kuwa wao ni watu safi na wapiganaji katika ujenzi wa “Dunia bora kwa wote”, watoto wa wafanyakazi hasa wale wenye kipato kilichotukuka na kubatizwa majina yenye kuchukiza!? Hawakuwa na njia nyingine zaidi ya kuingia katika mduara na kujifanya nao ni wachezaji wa mdundo wa “Utenzi wa watoto wa wakulima”.Watoto wa wakulima wakadanganyika na kufikiri ni wenzao.Wanaposhituka,tayari wachezaji wakuu wa utenzi huo ni wale wale “waliotengwa”-hatimaye wametekwa nyara!!.Ishara ya hali hiyo ni matokeo ya utendaji wa viongo wetu ambao awali tulidhani ni wenzetu???!!!

Wanazuoni!!!! Ikiwa bado tunaamini katika misingi ya waasisi wa taifa letu ya kuwa hii ni nchi ya wakulima na wafanyakazi.Basi huu ni wakati wetu muafaka kudurusu upya mantiki ya msamiati huu wa “ mtoto wa mkulima” ili kuupatia maana stahili katika wakati stahili. Katika kufanya hivyo ni budi tukajikita vema katika kuangalia vigezo tunavyovitumia kutambua motto wa mkulima au vinginevyo kama haja hiyo ipo na mantiki tunayoitumia katika kuwagawa “ watoto wa watanzania” katika madaraja/makundi hayo.

Binafsi, nafikiri huu ni wakati muafaka wa kuzungumzia “uzalendo” . Tuwazungumzie watoto wa wazalendo wa Tanzania [Wakulima: wadodo,wakati & wakubwa Na wafanyakazi: wa kima cha chini,kati na juu].Ikiwa msamiati wa “mtoto wa mkulima” tumekuwa tukilitumia kumpambambanua mtoto wa Mtanzania mwenye kipato cha chini basi hilo ni kosa kubwa ambalo hatuna budi kuacha kuendelea kulifanya haraka iwezekanavyo kwa kuwa sio kweli kuwa kila mtoto wa mkulima anatoka katika familia duni.Aidha,ikiwa msamiati huo tunautumia katka kuwapambanua “ wapiganaji” au wanaharakati wa vuguvugu la umajumuni basi huu ni wakati muafaka wa kutafuta msamiati sahihi baada ya msamiati wa “ mtoto wa mkulima kutekwa nyara!!!!.Hii ni nchi ya wakulima na wafanyakazi.

Kazi ya mja kunena
Mungu ibariki Afrika,

Mungu ibariki Tanzania!!!!!